
Na:
 Albert Sanga, Iringa.
Kumekuwa na changamoto kubwa kwa 
waliojiajiri na walioajiriwa kuhusu dhana ya mikopo na madeni. Licha ya 
kwamba wakati mmoja hadi mwingine, wengi wetu tumepata kuwa na mikopo au
 madeni; ni wachache wanaotambua maana halisi ya mikopo na madeni na 
namna mambo haya mawili yanavyotakiwa kwenda nayo katika maisha ya 
kiuchumi.
Tuchukulie mfano wa wafanyakazi. Wafanyakazi wengi huwa
 wanajikuta wakiishiwa mishahara yao kabla hata ya tarehe ya kupokea 
mshahara mwingine. Wakishamaliza mishahara yao huwa wanajikuta hawana 
namna ya kumudu bejeti zao, ikiwemo chakula na usafiri; hivyo wanapata 
mbinyo wa kuazima fedha, huduma au bidhaa kutoka kwa wenzao, katika 
maduka na kutoka kwa watu binafsi.
Wakishaazima hizo fedha, 
huduma au bidhaa; mioyo yao inasuuzika, wanamalizia siku zilizobaki 
kabla ya mshahara. Mshahara unapotoka wanajikuta wanatakiwa kulipa 
madeni yao, hivyo wengi wao huwa wanaanza kulipa yale madeni kisha 
inayobaki ndio wanaanza kutumia matumizi mengine. Mtindo unakuwa ni ule 
ule wa kuishiwa kabla ya mwisho wa mwezi. Kwa kadri mfanyakazi huyu 
anavyoendelea kukopa madeni kwa mtindo wa namna hii; anaendelea 
kuzalisha mfumo wa utegemezi unaokua. Ukifuatilia utabaini kuwa kama 
mwezi huu mshahara ulikuwa unaisha tarehe 20, basi mwezi  ujao utaisha 
tarehe 15, na unaofuata utakuwa unaisha tarehe 10!Mwisho wa siku 
mshahara wa mfanyakazi huyu usishangae kuona unaisha tarehe 2 ya mwezi! 
Kwa nini wafanyakazi na watu wengine waendelee kuishi maisha ya aina hii
 wakati fedha inapita mikononi mwao? Natambua wengi watasema tatizo ni 
kuwa mishahara wanayolipwa haitoshi, lakini ukweli ni kwamba tatizo 
kubwa ni kwamba, wengi hawaelewi namna ya kutumia fedha na jinsi ya 
kumudu madeni na mikopo.
Kanuni inasema kwamba kila fedha 
inayopita mkononi mwako unatakiwa kuichukulia kama mbegu. Ikipita 
shilingi kumi ni lazima itoke mikononi mwako ikiwa zaidi ya shilingi 
kumi. Hapo ndipo ilipo akili ya matumizi ya fedha. Kwa namna maisha 
yalivyo na halihalisi ya mishahara mingi ilivyo ni vigumu kukwepa suala 
la kukopa (na hata madeni).
Kwa ujumla hakuna ubaya wa kukopa, 
lakini kuna tofauti kati ya mkopo na deni. Mkopo ni fedha ama mali 
inayoazimwa kutoka kwa mtu ama kutoka kwa taasisi; kwa makubaliano ya 
kurejeshwa katika kipindi fulani; kwa madhumuni ya matumizi ya kuzalisha
 fedha zaidi ama mali zaidi. Wakati deni ni a) Fedha ama mali 
iliyoazimwa kwa ajili ya matumizi yasiyozalisha fedha ama mali zaidi b) 
deni ni mkopo uliopita muda wa makubaliano ya kulipwa.
Ndio maana
 mtu akienda kukopa fedha benki (kwa madhumuni ya kufanyia biashara) 
utasikia yule bwana ana mkopo, lakini akishindwa kurejesha mkopo ule kwa
 wakati uliopo kwenye makubaliano; utasikia yule bwana ana deni! Bahati 
mbaya ni kwamba kuna watu wengi sana ambao huwa wanachanganya kati ya 
deni na mkopo.
Wengi wana madeni lakini utasikia wanasema wana 
mikopo. Mtu anachukua fedha benki kwa dhamana ya mshahara wake kisha 
fedha hiyo anakwenda kununulia seti ya runinga, sofa na kununulia 
viwalo, halafu anajifariji kuwa ana mkopo, la hasha! Hilo ni deni. 
Wengine huchukua fedha benki na kununulia magari ya kutembelea nao 
hujifariji kwamba wana mikopo; sio kweli hawa ni kwamba wana madeni. 
Tena hawa wenye kuchukua fedha na kununulia magari ya kutembelea ambayo 
hayawaingizii chochote zaidi ya kuwalamba fedha zao; wanatakiwa kuyaita 
“madeni ya kutembelea” na sio magari ya kutembelea.
Katika nukta 
hii, namna nzuri ya kutumia fedha ni pamoja na kutambua vema nafasi ya 
mkopo na deni kwako. Unaamini nini kuhusu mikopo na madeni? Una uthubutu
 na tabia gani linapokuja suala la kudaiwa? Unahimili vipi madeni yako? 
Haya ni mambo ya kuyajua na kuyarekebisha yakae katika uelekeo sahihi 
kwa sababu yanaamua sana namna unavyoweza kutumia fedha zako.
Kukopa
 ni suala zuri sana. Biashara zote duniani zilianzishwa, haunzishwa na 
zitaendelea kuanzishwa kwa kutumia mikopo. Iwe umechukua hela mfukoni 
mwako na kuanzisha biashara huo ni mkopo, iwe umepewa fedha, huo ni 
mkopo kwa biashara yako.
Hata kama mkopo huo hauna riba wala 
hauhitaji kurudishwa hilo haliondoi uhalisia wa kwamba ni mkopo na 
katika mizania ya kihasibu mtaji wa kila biashara unatakiwa kuonesha 
kuwa mtaji wa mwanzo ni mkopo. Hata watu binafsi, iwe ni walioajiriwa 
ama laa, wenye cha kufanya ama wasio na cha kufanya; ukweli ni kwamba 
kuna wakati kwenye maisha utapungukiwa na utahitaji kukopa.
Unaweza 
kukopa benki, kwenye taasisi nyingine ama kwa mtu binafsi, kote huko ni 
kukopa. Imani yako kuhusu mikopo itaamua sana namna unavyotumia fedha 
zako katika kulipa ama kutokulipa. Bahati mbaya ni kwamba tunao 
watanzania wengi ambao hawataki hata kidogo kusikia habari za mikopo.
Hawa utawasikia wakisema, “Mikopo haina maana”, “Kukopa ni umasikini”, 
“Ukitaka kufilisika jaribu kukopa”. Kama muhusika anaamini hivi uwe na 
uhakika kwamba ufahamu wake utapeleka taarifa katika ubongo inayoonesha 
kwamba mkopo ni utumwa!
Sheria ya uvutano wa kimaumbile (Law of 
attraction) inasema kwamba chochote anachokiogopa mtu hutokea na 
chochote anachokiogopa mtu hukiabudu na chochote mtu anachokiabudu 
hudhihirika. Mtu anaeamini kuwa mikopo haifai ikitokea amekopa 
atakachojitahidi ni kuhakikisha kuwa anahangaika kuulipa mkopo huo ama 
deni hilo haraka haraka.
Ikiwa mtu huyu ni mfanyakazi ndio 
atarudi kule mwanzo ambapo kila akipata mshahara atakuwa anakimbilia 
kurejesha deni analodaiwa. Kinachotokea? Ni kwamba ataendelea kukopa 
tena na tena na kuendelea kuwa katika utumwa wa madeni na mwisho wa siku
 akishalemewa atajidhihirishia yeye mwenyewe imani yake ya kwamba kukopa
 ni utuwa na mateso.
Bahati mbaya wapo wazazi ambao huwaaminisha 
watoto wao tangu wakingali wadogo ama wakiwa makazini ya kwamba mikopo 
ni mibaya. Hata wale wanaokopa kupitia makato ya mishahara yao hawawi 
salama ikiwa wana imani mfu kuhusu mikopo na madeni. Kwa sababu 
aliyechukua mkopo na kwenda kununua gari ama kununua fenicha za ndani, 
siku mshahara unapoanza kukatwa na kujikuta haumtoshelezi atageuka na 
kuanza kunung’unikia madeni kwa ukali wa makato anayoyapata.
Nini
 maana yake mambo hayo ya madeni na mikopo? Kumbuka kwamba tunaangalia 
namna ya kuwa na matumizi mazuri ya fedha. Na nimesema kwamba matumizi 
mzuri ya fedha ni kutumia fedha katika mtiririko unaokuimarishia uchumi 
wako na sio kukudidimza.
Sasa, kuna wakati katika maisha unaweza 
kupitia katika changamoto ya madeni. Huenda ulichukua fedha eidha kwa 
mtu ama katika taasisi kwa lengo zuri la kuzalisha, lakini mambo 
yakaenda mrama na ukajikuta mkopo umegeuka kuwa deni na  huna namna ya 
kulipa kwa wakati husika. Lakini pia huenda ulichukua fedha na 
kuielekeza katika matumizi ya ‘kimadeni-madeni’ na unatakiwa kulipa. 
Walisema waswahili ya kwamba dawa ya deni ni kulipa; hilo ni kweli 
lakini unatakiwa kulipa deni lako na wakati huo huo uchumi wako 
uimarike.
Kama ulichukua mkopo benki kwa dhamana ya mali zako; 
hilo nitalileta kwa kina zaidi katika makala yenye kichwa, 
“Wajasiriamali na jinamizi la mikopo”. Lakini kote kote, iwe ni kutoka 
benki, iwe umekopa kwa mtu ama iwe umekopa dukani (na ukajikuta una 
deni) ni lazima sana uhakikishe unalipa kwa akili.
Kuchukua 
mshahara wote na kulipa madeni hakutakusaidia zaidi ya kukuangamiza. 
Kuchukua faida yote na kuipeleka kwa wadeni nako kutakuachia umasikini. 
Ukiwa katika hali hii ni lazima uzikumbuke tabia za kitajiri; 
kuhakikisha unatenga kwanza akiba kisha mengine yanafuatia.
Hata 
kama kuna mbinyo mkali kiasi gani ili ujikwamue na madeni ni lazima 
uhakikishe unatenga sehemu ya mshahara ama faida yako kwa ajili ya akiba
 (nap engine uwekezaji) na inayobaki ndipo iende kwa kulipa madeni na 
matumizi ya kawaida (yale matumizi yasiyozalisha). Kujua namna nzuri ya 
kutumia fedha ni pamoja na kuwa imara na mwenye msimamo dhidi ya 
wanaokudai.
Wanaokudai wanaweza kuwa na vishondo vikubwa kweli 
kweli, wanaweza kuwa na matisho makali kweli kweli, lakini muda wote 
jitahidi kuvumilia vishondo na matisho yao na kamwe matisho na vishindo 
vyao visikutoe kwenye kanuni hii, “Madeni yote yalipwe baada ya kutenga 
akiba”.
Kwa wale waamini wanaozingatia masuala ya sadaka, kanuni hii
 inanyumbuka na kuwa “Madeni yote yalipwe baada ya kutenga sadaka na 
akiba”. Madeni ni changamoto na ni kitu ambacho kinatakiwa kuchukuliwa 
kama kipindi cha mpito kwa mtu yeyote anaepambana kuimarisha uchumi 
wake.
Kwenye kitabu cha The Richest Man In Babylon; tunapewa maarifa
 kwamba haijalishi upo kwenye madeni makubwa na magumu kiasi gani, njia 
rahisi ya kujikomboa kiuchumi ni kuhakikisha unatenga si chini ya 
asilimia kumi ya kila fedha unayoipata; na kisha kuanza kuitumia ile 
fedha uliyotenga kwa ajili ya kuwekeza na kuzalisha. 
Sote tunastahili ushindi wa kifedha na kiuchumi.
#PoweredBySisiVijanaTanzania